Uncategorized

Siku za hatari kwa mwanamke.

Mzunguko wa hedhi huanzia siku ya kwanza ya kutoka kwa damu hadi siku ya kwanza tena ya kutoka damu ya mzunguko unaofuata. Japokuwa mzunguko wa hedhi wa kawaida ni siku 28, ni jambo la kawaida kuwa na mzunguko wenye siku pungufu au zaidi ya hizo.

Mzunguko huu huweza kutofautiana kati ya wanawake lakini pia kati ya mzunguko mmoja na mwingine. Mzunguko wa kawaida huwa na siku 21 hadi siku 35 kwa wanawake wakubwa na siku 21 hadi 45 kwa wasichana wadogo walioanza hedhi.

Kwa miaka michache ya awali baada ya msichana kupata hedhi yake ya kwanza (kuvunja ungo), kupata mizunguko mirefu huwa ni jambo la kawaida. Mizunguko huanza kupungua urefu (idadi ya siku) na kuanza kuwa ya kawaida kadri umri unavyosonga na mara nyingi mzunguko huwa kati ya siku 21 hadi 35.

Ni siku gani yai huachiliwa (ovulation)?
Mara nyingi wanawake huamini kuwa yai huachiliwa katikati ya mzunguko wa hedhi. Ukweli ni kwamba yai huachiliwa siku 12 hadi 16 kabla ya mzunguko unaofuata kuanza.

Kwahiyo, japokuwa kwa mwanamke mwenye mzunguko wa siku 28 yai lake laweza kuachiliwa katikati ya hedhi (kati ya siku ya 12 na 16), mwanamke mwenye mzunguko wa hedhi wenye siku 36 yai lake huachiliwa kati ya siku 20 na 24.

Kwa wanawake wenye mizinguko isiyobadilika sana, njia nzuri ya kukadiria siku ya yai kuachiliwa ni kutoa 16 kutoka kwenye jumla ya siku za mzunguko wake wote na baada ya kupata jibu, ajumlishe jawabu hilo na 4. Hii itampa siku ambayo yai huweza kuachiliwa.

Kwa mfano, mwanamke mwenye mzunguko wenye siku 22 mara nyingi yai lake huachiliwa kati ya siku ya 6 hadi 10 ya mzunguko wake (22-16=6, halafu 6+4=10).

Leave a Comment